www.Afyamtandao.org ni mtandao wa kompyuta ulioanzishwa na Tume ya Kikristo ya Huduma za Jamii (CSSC) kwa lengo la kuunganisha hospitali zote za CSSC katika mtandao wa tarakilishi ili kuwezesha ukusanyaji, uhifadhi na upashanaji wa taarifa na ubadilishanaji wa uzoefu na maarifa miongoni mwa watumishi wa afya na wadau wengine wa sekta ya afya.
Mradi huu ambao umeanzishwa kwa ufadhili wa Taasisi ya Kimataifa ya Uholanzi ya Mawasiliano na Maendeleo (IICD) ni sehemu ya mkakati wa CSSC wa kuimarisha ufanisi katika utoaji wa huduma za kinga na tiba katika hospitali zake kote nchiini kwa kutumia teknolojia hii ya habarí na mawasiliano (TEKNOHAMA).
Ni katika muktadha huo wa kuongeza ufanisi na kuimarisha shughuli zake za utafiti, ushauri elekezi,,ushawishi na uratibu ndiyo maana CSSC iliamua kuanzisha Mradi wa Afyamtandao kwa ajili ya Sekta ya Afya pamoja na CSSC Public Website kwa ajili ya mawasiliano na umma na dunia kwa jumla.Aidha, pamoja na mitandao hiyo ipo pia CSSC Intranet ambayo imeanzishwa mahsusi kwa ajili ya kuimarisha mawasiliano ndani ya CSSC pamoja na taasaisi zake kwa kutumia tekinolojia hii ya kisasa.
Chanzo cha www.Afyamtandao.org ni Mkutano wa Pamoja wa Washikadau wa Sekta ya Afya na Sekta ya Teknolojia ya Habarí na Mawasiliano uliofanyika mjini Mwanza,Februari 2005 kujadili namna ya kuwezesha matumizi ya TEKNOHAMA katika mfumo wa taarifa za uendeshaji wa shughuli za afya katika ngazi ya Wilaya.
Mkutano huo uliandaliwa kwa pamoja na Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii, CSSC na Tume ya Taifa ya Sayansi na Tekinolojia (COSTECH) kwa ushirikiano wa IICD na Netherlands Catholic Organization for Relief and Development Aid (CORDAID).
Mkutano huo ndio uliozaa mipango na maandalizi ya miradi ya ushirikiano miongoni mwa wadau hao kwa lengo la kushajiisha matumizi ya TEKNOHAMA katika kuleta mapinduzi ya kitekinolojia kwenye sekta ya afya.
Ingawa mradi wa Afyamtandao umeanzishwa na CSSC, matumizi yake ni kwa ajili ya washikadau wote wa sekta ya afya ndiyo maana katika Katiba yake mradi huu una kipengere cha Uanachama na vikao vya Wamiliki na Washikadau ambavyo ndivyo vitakavyoelekeza kuhusu sera na uendeshaji wake
CSSC ni chombo kilichoundwa mwaka 1992 kwa pamoja kati ya Kanisa Katoliki Tanzania (TEC) na Baraza la Kikristo Tanzania(CCT) kwa lengo la Kusimamia huduma za afya na elimu zinazotolewa na Makanisa hapa nchini. CSSC ilisajiliwa Januari 1993 na mwaka 1994 ikaandikishwa chini ya Sheria ya Wadhamini.
CSSC ni chombo kikubwa zaidi cha Dini hapa Afrika Mashariki kwa sifa kwamba kina Dayosisi na Majimbo 83 na kinamiliki na kuendesha asilimia 40 ya huduma a afya na asilimia 24 ya huduma za elimu zitolewazo hapa nchini. Habarrí zaidi kuhusu CSSC zinapatikana katika tovuti kwa anuani: www.cssc.or.tz