Kituo cha Mawasiliano Sengerema
Wilaya ya Sengerema iliyopo Mkoani Mwanza, inaendesha kituo cha mawasiliano kinachojulikana kama “Sengerema Multipurpose Community Telecentre”kwa lengo la kuwawezesha wananchi wa wilaya hiyo kupata taarifa kupitia Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEKNOHAMA) kwa njia rahisi.
Kituo hicho ambacho kimedhamria kuboresha Mawasiliano katika Wilaya hiyo,kinaendesha Redio ya jamii (Community Radio) ambayo inarusha matangazo yake ambayo yanawafikia wakazi wengi wa wilaya hiyo inayokadiriwa kuwa na idadi ya watu zaidi ya 615,000.
Mratibu wa Telecentre Bw.Falician Ncheye,anasema kuanzishwa kwa kituo hicho kulilenga zaidi kuunganisha makao makuu ya Wilaya na Ofisi za kata,shule za Sekondari,Vituo 5 vya afya vilivyopo katika wilaya hiyo,Chuo 1 cha Maendeleo ya jamii,Ofisi ya Kilimo wilaya,Ofisi ya mpango wa Maendeleo ya wajasiriamali wilaya,mtandao wa mashirika yasiyo ya kiserikali, Jumuiya ya walimu Tanzania,Shule za msingi na Sekondari Sengerema wilayani humo na watu binafsi kuweza kupata takwimu na habari mbalimbali ndani na nje ya nchi.
Bw.Ncheye anasema, kituo hicho kimefanikiwa kuboresha mawasiliano kwa njia ya Mtandao (internet) kwa baadhi ya maeneo huku wakiwa wamejipanga zaidi kuimarisha katika sehemu zingine ambazo bado zina matatizo.
Amesema wananchi wa Sengerema kwa sasa wanapata mawasiliano ya Mtandao(internet) kirahisi baada ya kuboresha mfumo wa wireless ambao umeanza kutumika katika baadhi ya vituo vya mjini wilayani hapo,huku kukiwa na mpango wa kufanya mfumo huo kuenea wilaya nzima.
Mratibu huyo amesema, mfumo wa kuunganishwa na wireless ni mzuri ambao una gharama ndogo ukilinganisha na mifumo mingine.