|
elearning
eLearning kwa Maendeleo ya Sekta Afya Tume ya Kikristu ya Huduma za Jamii (CSSC) kupitia mradi wa AfyaMtandao kwa kushirikiana na Taasisi ya Kimataifa ya Mawasiliano na Maendeleo (IICD),imefanya Warsha ya Masomo kwa njia ya TEKNOHAMA (eLearning) kwa lengo la kuboresha sekta ya Afya nchini.  Warsha hiyo ya siku moja ilifanyika hivi karibuni katika ukumbi wa baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania (TEC)-Kurasini Dar es salaam.
Lengo la Warsha hiyo iliyohusisha washiriki kutoka katika Taasisi za Afya nchini ilikuwa kujifunza kuhusu elearning jinsi inavyofanya kazi na kubadilishana utaalamu katika kuboresha na kuendeleza taaluma hiyo nchini Tanzania.
Katika warsha hiyo washiriki walijadili mambo muhimu ambayo yanapaswa kupewa kipao mbele ili kuzidi kuboresha huduma hiyo.Mambo hayo ni pamoja na kupandisha madaraja wahusika wa sekta hiyo kwenda kiwango cha juu,kuhamasisha wadau wa Afya kuhusu faida ya masomo hayo,kuainisha maeneo husika ya mafunzo,walengwa na mapato, na kuendeleza taaluma hiyo katika maeneo yote ya nchi.
Baadhi ya waratibu wa miradi walielezea miradi yao. Bw Petro Pamba Mratibu wa AfyaMtandao aliezea kuhusu AfyaMtandao jinsi inavyofanya kazi na mafanikio iliyoyapata tangu ilipoanzishwa Januari 2008,Bw.Dennis Mazali Mratibu wa eLearning aliuelezea mradi huo kwa washiriki jinsi unavyofanya kazi na changamoto zinazoukabili mradi huo.Naye Bi. Miep Lenoir kutoka shirika la IICD linalofadhili miradi hiyo aliwasilisha jinsi ambavyo Shirika lao linavyoshiriki kikamilifu katika kuboresha huduma za Afya kwa njia ya TEKNOHAMA.
Imewekwa: 24th Feb 09 na Renatus J Sona
|