|
Tathimini ya TEKNOHAMA hospitali ya Bulongwa
Tathimini ya TEKNOHAMA hospitali ya Bulongwa Timu ya CSSC- AfyaMtandao hivi karibuni ilifanya tathimini ya TEKNOHAMA katika hospitali ya Bulongwa kwa lengo la kuboresha huduma ya afya inayotolewa hospitalini hapo kwa njia ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEKNOHAMA).Katika zoezi hilo lililofanyika kwa wiki nzima, ilifahamika kuwa, hospitali hiyo ina Kompyuta za kutosha na baadhi ya maeneo tayari yana Soketi ambazo zinaweza kuunganisha Kompyuta hizo na mfumo maalumu wa kuhifadhi taarifa za wagonjwa (AfyaPro au Care2x). Maeneo hayo yaliyo na Soketi ni yale ya wagonjwa wanaokuja kutibiwa na kuondoka (Outpatient rooms) na yale ya wagonjwa wanaolazwa (Ipatient rooms), pia ofisi za utawala na uhasibu.
Tathimini hiyo pia imeonyesha kuwa, hospitali hiyo pia ina chumba maalumu cha Mtandao (Internet) ambacho kina Kompyuta tatu na kinatumiwa na watumishi wa hospitali hiyo kupata taarifa mbalimbali za afya.
Pamoja na kuwa na Kompyuta chache, hospitali hiyo inakabiliwa na tatizo la kuwa na watumishi wachache walio na uelewa wa kutumia Kompyuta, hivyo ilipendekezwa kuwa watumishi wengi wapewe mafunzo ya Kompyuta kwa kuanza kufundishwa hatua ya awali za namna ya kutumia Kompyuta.Pia katika tathimini hiyo, hospitali hiyo ilishauriwa kuanzisha tovuti yake ambayo itatumika kujitangaza na watu wengi kufahamu huduma zitolewazo na hospitali hiyo na kuajiri mtalaamu wa ufundi atakayesaidia kutatua matatizo mbalimbali ya Kompyuta.
Hospitali ya Bulongwa ni moja kati ya hospitali kongwe ambayo imefanikiwa katika kutoa huduma bora ya afya nchini Tanzania.Miongoni mwa mafanikio hayo ni pamoja na kutoa huduma ya Mtandao (Internet) kwa wakazi wa kijiji cha Bulongwa, kuongeza idadi ya wataalamu wa tiba kati yao ni madaktari wawili wa kigeni, na kujenga kituo cha watoto yatima.Pamoja na mafanikio hayo, hospitali hiyo inakabiliwa na changamoto mbalimbali ikiwa ni pamoja na miundombinu ya kufika hospitalini hapo kuwa hafifu, kutokuwa na gari maalumu la wagonjwa (Ambulance).Hospitali hiyo iko katika kijiji cha Bulongwa, wilaya ya Makete mkoa wa Iringa na ilianza kama Zahanati mwaka 1946 na ilipanda na kuwa hospitali mwaka 1968.
Imewekwa: 10th Sep 09 na Renatus sona
|