|
CSSC yaendelea kutengeneza filamu
CSSC yaendelea kutengeneza filamu za makala ya afya
Tume ya Kikristo ya huduma za jamii (CSSC) kupitia kitengo cha AfyaMtandao imeendelea kutengeneza filamu mbalimbali za makala ya afya, zinazoelezea mafanikio yanayotokana na huduma bora ya afya ambayo inatolewa na baadhi ya vituo vya afya, kwa lengo la kuinua na kuboresha huduma hiyo kwa wananchi hususani wanaoishi katika maeneo ya vijijini ambako huduma ya afya inakabiliwa na changamoto nyingi.
Mpaka sasa CSSC, imeishatengeneza filamu tano tofauti za makala ya afya zinazoonyesha mafanikio yatokanayo na huduma hiyo kutoka maeneo tofauti ya Tanzania, zikiwa zimelenga kuyafikia malengo ya millennia.Makala hizi ni; Mfumo wa kuhifadhi na kusimamia taarifa za afya za wilaya kwa njia ya Kompyuta (DHMIS), Kangaroo njia inayotumiwa na hospitali ya Sengerema katika kuwatunza watoto ambao hawajafikia uzito unaotakiwa na huduma ya TibaMtandao (Telemedicine) jinsi inavyofanyika kwa baadhi ya hospitali ambazo zinatumia tiba hiyo katika kanda ya kaskazini.
Filamu za kwanza kutengenezwa na CSSC mara tu baada ya kuanzisha kitengo chake cha kuzalisha filamu za makala ya afya ni; Ushirikiano wa wadau wa afya mkoani Rukwa na Mafanikio ya utoaji huduma ya afya mkoani Rukwa. Filamu hizo tayari zimekamilika na kusambazwa kwa wadau wa afya kwa lengo la kushirikisha mafanikio hayo.
Filamu hizo pia zimekuwa zikitumika katika mikutano mbalimbali ambayo imekuwa akiandaliwa na CSSC kwa lengo la kuhamasisha hospitali na wadau wengine kujifunza mafanikio hayo. Kwa sasa CSSC iko katika hatua za mwisho za kutoa makala nyingine ya filamu inayohusu mfumo wa ukusanyaji na usimamizi wa taarifa za afya kwa njia ya Kompyuta ambao unatumia “Software” ya Care2x. Filamu hii imetengenezwa mkoani Arusha ambako mfumo huu unafanya kwenye baadhi ya hospitali.
CSSC ilianzisha kitengo cha kutengeneza filamu kwa lengo la kutangaza na kushirikishana mafanikio yanayofanywa na vituo vya afya katika sekta ya afya nchini Tanzania.
Imewekwa: 24th Nov 09 na Renatus Sona
|