|
Suala la Rasilimali watu ni tatizo
Suala la Rasilimali watu ni tatizo-Dk.Adeline Kimambo
Imeelezwa kuwa sekta binafsi kwa kushirikiana na Serikali inajukumu kubwa la kutatua tatizo la Rasilimali watu ili kutoa huduma bora isiyokuwa ya ushindani baina ya watoa huduma wa sekta binafsi na Serikali.
Hayo yamebainishwa na mkurugenzi wa Tume ya Kikristo ya huduma za jamii (CSSC) Dk.Adeline Kimambo kwenye mkutano wa uzinduzi wa kamati maalumu itakayosimamia mradi wa Rasilimali watu Tanzania ambao umeanza kutekelezwa na Tume hiyo kupitia kitengo cha AfyaMtandao.
Dk. Kimambo ameeleza kuwa suala la Rasilimali watu ni tatizo kutokana na kuwa hakuna mfumo ambao unatumika kutunza takwimu za watumishi hivyo inakuwa ngumu kwa hospitali kujua idadi ya watumishi iliyonao, kada na elimu zao.
CSSC kwa kushirikiana na wadau wengine ikaona kuna umuhimu wa kutatua tatizo hilo kwa kuanzisha mfumo ambao utawezesha kutambua na kuzipata takwimu sahihi za watumishi hivyo ikaona ni bora kuanzisha mradi huu ili hospitali za taasisi za dini, Serikali na zile za binafsi zianze kutumia mfumo huo.
Aidha Dk.Kimambo amebainisha kuwa ili kufanikisha azima hii ya kuwa na mfumo huo, ushirikiano wa pamoja baina ya Serikali, taasisi za dini na sekta binafsi ni muhimu sana katika kuboresha huduma ya afya kwa kufanikisha utekelezaji wa mradi.
Mradi wa Rasilimali watu ni wa miaka minne na umeanza kutekelezwa na CSSC mwezi Septemba mwaka jana, na mwaka wa kwanza ni wa uhamasishaji kwa wadau kuelewa mfumo wenyewe jinsi utakavyofanya kazi ambapo CSSC inashirikiana na wadau wengine wa afya ambao ni umoja wa watoa huduma ya afya binafsi (APHFTA) na Baraza la waislamu Tanzania (Bakwata). Mkutano wa uzinduzi wa kamati hiyo ulifanyika Kibaha Pwani na mradi huu unafadhiliwa na watu wa Marekani kupitia shirika la IntraHealth-Tanzania.
Imewekwa: 6th Jan 10 na Renatus sona
|