|
Mradi wa Rasilimali watu katika sekta ya afya
Sekta binafsi inamchango mkubwa katika Sekta ya Afya IMEELEZWA kuwa sekta binafsi inamchango mkubwa katika sekta ya afya endapo ushirikano baina ya watoa huduma binafsi, makanisa na Serikali utazidi kuimarika.
Akizungumza katika mkutano wa siku mbili uliyowakutanisha wadau wa sekta ya afya, Mkurugenzi wa Tume ya Kikristo ya Huduma za Jamii (CSSC) Dkt. Adeline Kimambo amesema ushirikiano uliyopo baina ya Serikali na Sekta binafsi ni mzuri, ambapo kwa sasa Serikali kupitia baadhi ya halmashauri za wilaya zimeanza kuajili watumishi na kuwapeleka kwenye hospitali zinazomilikiwa na Taasisi za dini ili kukabiliana na tatizo la upungufu wa watumishi ambalo kwa sasa ni kubwa katika hospitali hizo.
“Uhaba wa watumishi katika sekta ya afya ni tatizo kubwa zaidi katika hospitali za binafsi, hata hivyo juhudi za pamoja zimekuwa zikifanyika kuhakikisha kuwa tatizo hilo linatatuliwa ambapo tayari baadhi ya halmashauri za wilaya zimeanza kuajili watumishi na kuwapeleka kufanya kazi katika hospitali za taasisi za dini.” Alisema.
Aidha katika kutekeleza azima ya ushirikiano huo unaojulikana kama Public Private Partnership (PPP), Dkt. Kimambo ameeleza kuwa tayari kuna vituo 7 vya afya vinavyomilikwa na makanisa vimesaini mkataba wa utoaji huduma ya afya na halmashauri za wilaya hali ambayo itapelekea huduma hiyo kuimarika, na kutoa wito kwa halmashauri zingine kuingia katika mpango huo.
Katika hatua za kukabiliana na tatizo hili, CSSC kwa kushirikiana na shirika lingine la Intrahealth kwa ufadhili wa shirika la misaada la marekani (USAID), imeanzisha mradi wa Rasilimali watu ambao unaainisha na kutambua idadi ya watumishi, kada, na elimu zao.
Naye mratibu wa mradi huo Bw. Petro Pamba amesema kuwa mkutano huo umelenga kuboresha matumizi ya Sera na Miongozi iliyopo ya Rasilimali watu katika Sekta ya Afya, kutambua mahitaji ya watumishi yanayotakiwa ili kuwajengea uwezo kwa kuwaendeleza.
Bw Pamba amesema mfumo wa Rasilimali watu unatumika kutunza takwimu za watumishi kwa njia ya Mtandao wa Kompyuta hivyo inakuwa rahisi kwa hospitali kujua idadi ya watumishi iliyonao, kada na elimu zao.
Awali akifungua mkutano huo, kwa niaba ya Katibu mkuu wa Baraza la maaskofu Katoliki Tanzania (TEC), Musinyori Julian Kangalawe, amesema makanisa yamekuwa mstari wa mbele katika kutoa huduma ya afya nchini ambapo mafanikio yanaonekana kutokana na huduma nzuri itolewayo na hospitali za rufaa za Bugando na KCMC zinazomilikiwa na makanisa.
Pamoja na hayo Musinyori Kangalawe amesema kuwa hivi sasa nchi inauhaba wa rasilimali watu 32,000 ambayo ni sawa na asilimia 61, huku takwimu za hivi karibuni zikionyesha kuwa nchi ina madaktari 1339 pamoja na wale wa kwenye sekta binafsi 455, hivyo kufanya daktari 1 kuhudumia wagonjwa 25,000.
Tume ya Kikristo ya huduma za jamii (CSSC) ni chombo cha pamoja kati ya Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania (TEC) na Baraza la Kikristo Tanzania (CCT) kilichoundwa mwaka 1992 kwa lengo la kusaidia huduma za jamii kwa upande wa Afya na Elimu kupitia hospitali na shule zinazomilikiwa na makanisa.
Imewekwa: 5th Feb 10 na Renatus sona
|