|
Hospitali yapunguza vifo vya watoto
Hospitali yapunguza vifo vya watoto HOSPITALI ya Mkoa wa Singida imepunguza idadi ya vifo vya watoto wachanga wenye umri chini ya miaka mitano wanaozaliwa hospitalini hapo kutoka watoto 138 mwaka 2006 hadi kufikia watoto 75 Septemba mwaka jana.
Akizungumzia mikakati ya kukabiliana na vifo hivyo vya watoto wachanga chini ya miaka mitano, Mganga Mkuu wa Mkoa wa Singida, Dk. Robert Salimu, aliitaja kuwa ni pamoja na kuongeza idadi ya watumishi wenye ujuzi, hususan daktari bingwa wa magonjwa ya watoto na wauguzi wenye ujuzi.
Kwa mujibu daktari huyo kutokana na kukosekana kwa daktari bingwa kwa sasa, mahitaji ya hospitali ni kuwa na madaktari bingwa wanne wa magonjwa ya watoto, madaktari 17 na wauguzi wakunga 250.
“Kutokana na hospitali ya mkoa kutokuwa na daktari bingwa wa magonjwa ya watoto kwa sasa, kunahitajika madaktari bingwa wa aina hiyo wanne, madaktari 24 waliopo ni 8 hivyo kuwepo upungufu wa 17 na wauguzi wakunga ni 250 kati ya 360 wanaohitajika katika hospitali hii,” alifafanua.
Kwa mujibu wa mganga mkuu huyo mikakati mingine ni pamoja na kupanua chumba maalumu cha kuhudumia watoto wachanga, kuhakikisha watoto wanakamilisha ratiba za chanjo, utumiaji wa vidonge vya Vitamini A na dawa za minyoo, kutoa mafunzo ya kumsaidia mtoto mchanga kupumua, watumishi watatu wamepatiwa mafunzo hayo na kuendelea kutoa elimu kuhusu dalili za hatari katika jamii.
Mikakati mingine ni kuhakikisha watoto waliozaliwa na VVU wanachukuliwa sampuli mapema na kupatiwa tiba ambapo watumishi watatu wamepatiwa mafunzo ya kuchukua na kusafirisha sampuli katika Hospitali ya Bugando, kununua vifaa vya kisasa vya kutolea huduma kama vile kitanda kwa ajili ya huduma za dharura, kutoa mafunzo kwa watumishi wa hospitali ya mkoa kuhusu tiba mseto (IMCI) ambapo tayari watumishi 9 wameshapatiwa mafunzo hayo kati ya lengo la watumishi 120 wanaotarajiwa kunufaika na mpango huo.
Imewekwa: 16th Feb 10 na Renatus sona
|